Zaburi 93

1 Mwenyezi Mungu anatawala, amejivika utukufu; Mwenyezi Mungu amejivika utukufu tena amejivika nguvu. Dunia imewekwa imara, haitaondoshwa.

2 Kiti chako cha enzi kimekuwa thabiti tangu zamani; wewe umekuwa tangu milele.

3 Bahari zimepaza, Ee Mwenyezi Mungu, bahari zimepaza sauti zake; bahari zimepaza sauti za mawimbi yake.

4 Yeye ni mkuu kuliko ngurumo ya maji makuu, ni mkuu kuliko mawimbi ya bahari: Mwenyezi Mungu aishiye juu sana ni mkuu.

5 Ee Mwenyezi Mungu, sheria zako ni imara; utakatifu umepamba nyumba yako pasipo mwisho.