Zaburi 65

1 Ee Mungu, sifa zakungojea katika Sayuni; kwako wewe nadhiri zetu zitatimizwa.

2 Ewe usikiaye maombi, watu wote watakuja kwako wewe.

3 Tulipokuwa tumefunikwa kabisa na dhambi, wewe ulisamehe makosa yetu.

4 Heri wale uliowachagua na kuwaleta karibu ili waishi katika nyua zako! Tunashibishwa kwa mema ya nyumba yako, mema ya Hekalu lako takatifu.

5 Unatujibu kwa matendo ya kushangaza ya haki, Ee Mungu Mwokozi wetu, tumaini la miisho yote ya duniani na la bahari zilizo mbali sana,

6 uliyeumba milima kwa uwezo wako, ukiwa umejivika nguvu,

7 uliyenyamazisha dhoruba za bahari, ngurumo za mawimbi yake, na ghasia za mataifa.

8 Wale wanaoishi mbali sana wanaogopa maajabu yako, kule asubuhi ipambazukiapo na kule jioni inakofifilia umeziita nyimbo za furaha.

9 Waitunza nchi na kuinyeshea, waitajirisha kwa wingi. Vijito vya Mungu vimejaa maji ili kuwapa watu nafaka, kwa maana wewe umeviamuru.

10 Umeilowesha mifereji yake na kusawazisha kingo zake; umeilainisha kwa manyunyu na kuibariki mimea yake.

11 Umeuvika mwaka taji la baraka, magari yako yanafurika kwa wingi.

12 Mbuga za majani za jangwani umezineemesha; vilima vimevikwa furaha.

13 Malisho yamejaa makundi ya wanyama, na mabonde yamepambwa kwa mavuno; vyote vinashangilia kwa furaha na kuimba.