Zaburi 43
1 Ee Mungu unihukumu, nitetee dhidi ya taifa lisilomcha Mungu, niokoe na watu wadanganyifu na waovu.
2 Wewe ni Mungu ngome yangu. Kwa nini umenikataa? Kwa nini niendelee kuomboleza, nikidhulumiwa na adui?
3 Tuma hima nuru yako na kweli yako viniongoze; na vinilete hadi mlima wako mtakatifu, mahali unapoishi.
4 Ndipo nitaenda madhabahuni pa Mungu, kwa Mungu, furaha yangu na shangwe yangu. Nitakusifu kwa kinubi, Ee Mungu, Mungu wangu.
5 Ee nafsi yangu, kwa nini unasononeka? Kwa nini unafadhaika hivyo ndani yangu? Weka tumaini lako kwa Mungu, kwa sababu bado nitamsifu Mwokozi wangu na Mungu wangu.