Zaburi 16
1 Ee Mungu, uniweke salama, kwa maana kwako nimekimbilia.
2 Nilimwambia Mwenyezi Mungu, “Wewe ndiwe Bwana wangu; pasipo wewe sina jambo jema.”
3 Kuhusu watakatifu walio duniani, hao ndio wenye fahari, na ninapendezwa nao.
4 Huzuni itaongezeka kwa wale wanaokimbilia miungu mingine. Sitazimimina sadaka za damu kwa miungu kama hiyo, au kutaja majina yao mdomoni mwangu.
5 Mwenyezi Mungu umeniwekea fungu langu na kikombe changu; umeyafanya mambo yangu yote yawe salama.
6 Alama za mipaka zimeniangukia mahali pazuri, hakika nimepata urithi mzuri.
7 Nitamsifu Mwenyezi Mungu ambaye hunishauri, hata wakati wa usiku moyo wangu hunifundisha.
8 Nimemweka Mwenyezi Mungu mbele yangu daima. Kwa sababu yuko mkono wangu wa kuume, sitatikisika.
9 Kwa hiyo moyo wangu unafurahia, na ulimi wangu unashangilia; mwili wangu nao utapumzika salama,
10 kwa maana hutaniacha Kuzimu, wala hutamwacha Mtakatifu Wako kuona uharibifu.
11 Umenijulisha njia ya uzima; utanijaza na furaha mbele zako, pamoja na furaha ya milele katika mkono wako wa kuume.