Zaburi 146

1 Msifuni Mwenyezi Mungu! Ee nafsi yangu, umsifu Mwenyezi Mungu,

2 Nitamsifu Mwenyezi Mungu maisha yangu yote; nitamwimbia Mungu wangu sifa wakati wote ningali hai.

3 Usiweke tumaini lako kwa wakuu, kwa wanadamu ambao hufa, ambao hawawezi kuokoa.

4 Roho yao itokapo hurudi mavumbini, siku hiyo hiyo mipango yao yote hukoma.

5 Heri yeye ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, ambaye tumaini lake ni katika Mwenyezi Mungu, Mungu wake,

6 Muumba wa mbingu na nchi, na bahari na vyote vilivyomo: Mwenyezi Mungu anayedumu kuwa mwaminifu milele na milele.

7 Naye huwapatia haki waliodhulumiwa, na kuwapa wenye njaa chakula. Mwenyezi Mungu huwaweka wafungwa huru,

8 Mwenyezi Mungu huwafumbua vipofu macho, Mwenyezi Mungu huwainua waliolemewa na mizigo yao, Mwenyezi Mungu huwapenda wenye haki.

9 Mwenyezi Mungu huwalinda wageni na kuwategemeza yatima na wajane, lakini hupinga njia za waovu.

10 Mwenyezi Mungu atamiliki milele, Mungu wako, ee Sayuni, kwa vizazi vyote. Msifuni Mwenyezi Mungu.